Ads 468x60px

.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

FOLLOW US ON TWITTER

FOLLOW US ON TWITTER

.

Tuesday, August 21, 2012

NJIA ZA KUFANIKIWA MAISHA KUPITIA HEKMA ZA MFALME SULEIMAN..

10:1-22:16  MITHALIZA SULEMANI
Mithali katika sehemu hii kwa jumla zimeandikwa kwa utunzi rahisi wa mistari miwili miwili, na karibu kila mithali inafanana na mstari fulani katika Biblia yetu. Ingawa mhariri aliyekusanya mithali hizo alijitahidi kujumlisha mithali zile zinazohusika na somo moja au maana maalumu, inafaa kila mithali ifikiriwe kwa ujumbe wake.

Ni wazi kwamba hapa hatuna nafasi ya kueleza kila mithali peke yake. Msomaji anapata faida zaidi akisoma kitabu cha Mithali pole pole na kwa uangalifu (kwa mfano fungu moja tu kwa wakati mmoja, ili aweke nafasi ya kutosha kati ya mafungu mbalimbali), akitulia na kuzingatia kila mithali na jinsi inavyohusika katika maisha ya kila siku. Mithali hizo ni mifano mizuri jinsi hekima na ujinga vilivyoelezwa katika mafungu ya 1-9, na vinavyoweza kuingizwa katika mazoea ya kila siku.

Hekima katika maisha ya kila siku (10:1-32)
Mkusanyo unafunguliwa kwa maelezo ya baadhi ya mawazo makuu ya sehemu zilizopita, yaani hekima na ujinga, haki na uovu, uvivu na bidii; kwa kutilia mkazo juu ya matokeo ambayo mambo hayo yanaleta kwa mtu binafsi na kwa watu wanaoishi karibu naye (10:1-5). Matendo ya mtu yanaonyesha tabia yake, ikiwa ni njema au mbaya, na sifa yake itaendelea hata baada ya kufa kwake (6-7). Mtu hujenga hekima kwa njia ya kujifunza, wala si kwa njia ya kujisifu. Anapata usalama kutokana na maisha ya unyofu, wala si kwa njia ya shughuli za hila (8-9).

Kuna watu ambao kwa njia ya matendo ya hila na maneno ya ujanja wanachokoza matata. Kuna wengine ambao kwa kusema wazi na kwa upendo huleta amani (10-12). Mwenye hekima hutunza ujuzi wake ili autumie wakati ufaao; lakini mpumbavu husema wakati usiofaa, na hivyo mara nyingi hujipatia shida (13-14).

Kwa muda fulani fedha zinaweza kuongeza usalama wa mtu, lakini lazima zipatikane kwa njia ya halali na zitumiwe kwa akili, kama inatakiwa ziongeze thamani ya maisha (15-17). Mtu akiwa na chuki moyoni mwake, maneno yake huwa na unafiki au yanachokoza. Afadhali maneno yake yawe kweli,
yaliyochaguliwa vizuri ili yawasaidie wasikilizaji (18-21).

Wapumbavu na wajeuri hujenga maisha yao juu ya vitu viharibikavyo na vya muda mfupi, kwa hiyo wanaogopa sana misiba ya ghafla inayoweza kuwaangamiza. Lakini kwa kweli mambo hayo yatawapata. Wenye haki wanajenga maisha yao juu ya mambo yanayodumu. Kwa hiyo wanaendelea kuwa na usalama na utulivu, ingawa wanaweza kukabiliwa na matatizo (22-25). Mvivu ni chukizo kwa mwajiri wake (26).

Mungu anaahidi maisha marefu, furaha na ulinzi wake kwa watu wenye haki. Anawahakikishia waovu kwamba, akichukua hatua dhidi yao, maisha yao yatakwisha katika hali ya kukatisha tamaa (27-30). Usemi wa wenye haki una hekima na wema, lakini ule wa waovu unadanganya na kuumiza (31-32).

Mafanikio, unyofu na utu wema (11:1-31)
Ni ujinga mtu akijaribu kutajirika kwa mbinu zisizo na haki, kwa sababu ukosefu wa uaminifu huleta hukumu wala mali haiwezi kumwokoa (11:1-4). Mtu asiyekuwa na hatia ana uhakika wa kupata ushindi wa mwisho, ila mwenye ujeuri hujiangusha mwenyewe (5-8). Watu wema wakiwa na sauti katika utawala wa mji, wenyeji wake huishi katika usalama na furaha, lakini kila mji una watu waovu wachokozao matata baina ya majirani na kuanzisha wasiwasi katika jumuia (9-11). Kwa sababu ya matatizo yanayoletwa na watu hao kwa usemi wao mbaya, viongozi wanapaswa kuweka sheria safi na yenye hekima (12-14).

Onyo lingine linatolewa kuhusu utoaji wa dhamana ya haraka (15; taz. maelezo ya 6:1-5). Ujeuri unaweza kuleta mafanikio, lakini utajiri huo hauaminiki, kwa sababu una muda mfupi tu. Kinyume chake, utu mwema huleta heshima ya kweli na thawabu inayodumu (16-20). Mungu anatawala maisha ya watu wote, naye anahakikisha kwamba maisha ya wenye haki tu ni maisha yenye maana (19-20). Kwa watu wengine tofauti zinaonekana kati ya maisha yao ya ndani na hali zinazoonekana nje, lakini mwisho haki itashinda (21-23).

Matokeo ya fadhili hayatakuwa umaskini, kwa sababu Mungu atatoa thawabu yake. Lakini watu wanawalaani wale ambao wakati wa njaa kali wanaficha chakula kwa makusudi ya kupandisha bei yake (24-26). Haidhuru mtu anatazamia kitu gani, ikiwa ni wema au ubaya, atakipata, lakini akitafuta usalama  kwa   njia   ya  kukusanya  mali   nyingi atakatishwa tamaa (27-29). Mwenye haki kwa maisha yake mema huleta baraka kwa watu wengine. Iwapo hata yeye mara nyingine anapata taabu kutokana na hukumu ya haki ya Mungu, zaidi sana mtu mwovu atapata shida kali mno (30-31).

Maneno ya kweli na kazi yenye haki (12:1-28)
Kuna mithali nyingine juu ya tabia ya kuvumilia lawama au kutaja makosa ya watu (12:1-2; taz. maelezo ya 9:7-9), juu ya maisha imara ya mwenye haki (3) na thamani ya mke mwema (4). Mtu mwenye haki, licha ya kuwa na kanuni safi, pia ana ujasiri wa kusema wazi bila ya kuogopa kujihatarisha, ili aweze kuwaokoa watu wengine (5-7).

Watu wakiishi katika unyenyekevu kadiri ya uwezo wao wa kujimudu, labda watakosa kupata sifa ya kuwa na hali ya juu, lakini wanaishi bila deni. Wana hekima kuliko wale wanaotumia pesa ovyo, ili kujivuna mbele ya watu wengine, lakini mwisho wana njaa na umaskini (8-9). Hali kadhalika ni afadhali watu wakihakikisha usalama wao kwa njia ya kufanya kazi ngumu, kuliko kupoteza wakati na fedha kwa mambo yasiyofaa. Kazi ya uaminifu na usemi wa kweli huheshimiwa na watu na kuwaridhisha wenye tabia hiyo (10-14).

Watu wenye busara husikiliza ushauri na kudharau maneno ya kuwaaibisha (15-16). Daima husema yaliyo kweli, lakini maneno yao husaidia na kuponya kuliko kuumiza (17-19). Wakifanya hivyo wanampendeza Mungu na kujaza furaha moyoni mwao (20-22). Wenye busara hukaa kimya kuliko kuonyesha ujuzi wao bure, lakini siku zote watakuwa na neno la kufaa kwa kumtia mtu moyo na kumwongoza anayehitaji msaada kama huo (23-26). Kinyume chake wavivu, kamwe hawapati wanachotaka, nao wanaweza kutawaliwa na wengine (23-28).

Kuridhika katika ugumu wa maisha (13:1-25)
Ushauri unaotolewa na wazazi ni jambo bora katika maisha. Watu wakataao ushauri huo daima, hujenga tabia ya kudharau mashauri yote isipokuwa yao wenyewe tu (13:1). Maneno mema huleta thawabu, lakini matokeo ya maneno ya hila ni ujeuri. Nidhamu katika usemi ni muhimu, kwa sababu maneno makali huleta uharibifu (2-3). Nidhamu pia inatakiwa katika kazi na maisha yote, la sivyo maisha ya mtu huishia katika uharibifu. Usalama hupatikana katika uaminifu (4-6).

Mara nyingine maskini anaweza kujionyesha kana kwamba ni tajiri (kwa sababu kuna faida fulani katika mali), lakini matajiri, kwa sababu ya ubahili, wanaweza kujionyesha kana kwamba ni maskini (7-8). Watu wakipata utajiri haraka, mara nyingi wanatumia mali yao bila uangalifu. Mali iliyopatikana pole pole kutokana na kazi ngumu inadumu zaidi (9-11).

Watu wakiona matarajio yao yakitimizwa wanafurahi; wakikubali mafundisho ya wenye hekima wataburudishwa (12-14). Wakiwa na akili safi ya kawaida wataheshimiwa na watu na wenyewe watafurahi. Watapata matarajio yao. Lakini wapumbavu hawana akili ya kutosha kwa kuficha ujinga wao wala kwa kuepukana na njia zinazowaletea uharibifu (15-19). Kufanikiwa katika maisha kunategemea sana watu ambao mtu anashirikiana nao (20-21).

Inaonekana kama kuna haki fulani, iwapo matajiri waovu wanapotelewa na mali yao waliyojipatia kwa njia ya kuwanyanyasa maskini. Ingawa kwa kawaida dhuluma inapinduliwa siku moja, wazazi hawana budi kuamua mashauri yao kwa haki iwezekanavyo wakati huo wanapowafundisha watoto wao na kuwaandaa kwa siku za usoni (22-25).

Hisia, tabia na makusudi (14:1-35)
Hekima hujenga, lakini ujinga hubomoa. Tabia ya mtu ya kumheshimu Mungu hudhihirishwa kwa matendo yake (14:1-2). Kati ya mambo yanayoamua kama mtu atakuwa na maendeleo mazuri au atafilisika ni hekima katika usemi wake na tabia yake kuhusu kazi ngumu (3-5). Mtu anayefikiri kwamba anajua mambo yote, kamwe hawezi kuwa na hekima ya kweli, na hivyo hatakuwa na utambuzi mzuri kuhusu maadili mema ya maisha (6-8).

Watu wema wanaweza kufanikiwa na waovu wanaweza kupata hasara, lakini moyoni mwa mtu, hata akiwa mwema sana, huzuni fulani inaweza kufichika ambayo hakuna mtu awezaye kuishiriki (9-14). Mtu aaminiye kila neno, atupaye mbali tahadhari yo yote, au afanyaye mambo yake kwa tabia ya harara, anazidisha shida ya ujinga wake tu (15-18). Mtu mwovu anaweza kuwaheshimu watu wema moyoni mwake, lakini anawadharau kabisa maskini, kwa sababu anajua kwamba hawezi kupata kitukwao (19-21).

Mithali tano zinazofuata zinahamasisha makusudi safi, bidii ya kazi, hekima, usemi wenye ukweli na heshima kwa Mungu (22-27). Hakuna mtu awezaye kuishi bila ya kuwategemea wengine; hata mfalme hawezi kuishi bila raia zake (28). Tabia mbaya inaharibu afya ya mtu pamoja na utu wake wa ndani, lakini unyanyasaji wa maskini huharibu uhusiano wake na Mungu (29-31). Hekima na haki huleta faida katika kila hali zinapotumiwa, ikiwa ni katika maisha ya binafsi au katika mambo ya siasa ya taifa lote (32-35).

Kuwafurahisha watu wengine (15:1-33)
Maneno yanaweza kuwafurahisha watu au kuwachokoza; kuwasaidia au kuwarudisha nyuma. Kwa hiyo ni muhimu sana mtu afikiri vizuri maneno anayotumia (15:1-5). Licha ya kuwa na busara katika usemi wake, lazima mtu awe na uaminifu katika njia za kujipatia riziki yake (6-7). Kwa kweli, hana budi kuwa mnyofu katika sehemu zote za maisha yake. Hapo tu Mungu ambaye mbele yake hakuna linalofichika, atapokea sadaka zake na maombi yake (8-11). Jambo lingine linalohusu usemi wa mtu ni kwamba, yule ambaye hupenda sana kuwaonya wengine, mara nyingi hukasirika akionywa mwenyewe (12).

Furaha ya moyoni humwezesha mwamini achangamke hata akiwa katika matatizo. Kwa kuwa anamcha Mungu kwa kweli na kuwapenda watu wengine, anaridhika hata asipokuwa na mali (13-17). Mfululizo wa maonyo unaonyesha kwamba matendo mabaya huleta taabu kubwa: tabia ya hasira huleta mabishano (18), uvivu humlazimisha mtu afanye kazi ngumu zaidi baadaye (19), ujinga huleta ugomvi nyumbani (20) na matokeo ya upumbavu ni kuharibika kwa mipango (21-22).

Watu wanaowafurahisha wengine wanahakikishiwa kupata wema wa Mungu (23-24), lakini Mungu huwapinga wale wanaofanya fitina na wanaotumia daraja lao la juu ili kuwanyanyasa maskini na wasioweza kujitetea (25-29). Sura ya mtu anayechangamka ni kama habari njema inayowaburudisha watu (30). Kitabu kinaendelea kueleza kwamba, ili kupata hekima watu hawana budi kujifunza, wamheshimu Mungu na wawe na roho yenye unyenyekevu (31-33).

Kupanga mikakati na uamuzi (16:1-33)
Mtu anaweza kuwa na maarifa na kupanga mikakati, lakini ni Mungu tu aamuaye matokeo yake, kwa sababu Yeye anajua hisia za mtu na kutawala matukio kadiri ya makusudi yake mwenyewe. Kwa hiyo ni muhimu kabisa kumwingiza Mungu katika mipango yote (16:1-4). Mungu anawaadhibu wenye kiburi na kuwahurumia waaminifu (5-6). Anawalinda wasipate shida na kuwaongoza katika njia za haki (7-9).

Iwapo hekima ya mfalme hutoka kwa Mungu, maamuzi yake huwa ya haki. Hataonyesha upendeleo, bali ataadhibu uovu, atasifu wema na kuangalia kwamba biashara zote zinaendeshwa kwa haki na amani (10-15). Tajiri wa kweli si mtu aliye na fedha nyingi, bali ni yeye aliye na hekima, unyofu, unyenyekevu, utiifu na uaminifu (16-20).

Usemi mwema hauna unafiki kama umetoka katika moyo safi. Unampa faida msemaji wake kwa sababu unayapa maneno yake ushawishi mwema na kuwapa wasikilizaji faida ya kujenga mawazo yao (21-24). Mtu anaweza kujidanganya mwenyewe, lakini hawezi kuepukana na ukweli kwamba asipofanya kazi, atalala na njaa (25-26). Kinyume cha usemi mwema uliotajwa sasa hivi, kunong'ona na kutoa mashauri ya ujanja huleta matata tu (27-30). Kuishi maisha ya unyofu huthibitisha heshima katika uzee. Kujitawala huthibitisha nguvu, na kuweka mambo yote mbele ya Mungu humpa mtu uamuzi uliosawa (31-33).

Marafiki na wajinga (17:1-28)
Maisha ya amani katika nyumba ni baraka kubwa, haidhuru watu wake wakiwa na hali ya chini; lakini mwana anaweza kukosa urithi wa familia yake kwa sababu ya ujinga wake (17:1-2). Matendo ya Mungu na watu wake siku zote yana makusudi mema, ili kuwafanya kuwa wema kuliko walivyokuwa awali (3). Kusikiliza maneno mabaya ni vibaya sawa sawa na kuyasema mwenyewe; kufurahia matatizo ya watu wengine ni vibaya sawa sawa na kuyasababisha mwenyewe (4-5).

Mithali nyingine zinahusika na uhusiano mwema ambao wazee na vijana wanapaswa kuwa nao (6), umuhimu wa usemi unaofaa (7), mafanikio yanayopatikana rahisi kwa kutoa rushwa isivyo halali (8), na tabia mbalimbali za wapatanishi na waletao ugomvi (9).

Wapumbavu ni watu wa hatari, kwa sababu ni wakaidi na waasi wala mtu hawezi kujadiliana nao (10-13). Kwao kutoelewana kidogo kunaweza kuchokoza ugomvi mkubwa. Wanafikiri kwamba wakimlipa mwalimu ada yake, wamekwisha pata hekima, lakini hawana nia ya kujifunza neno (14-16).

Mtu akiwa na shida anaweza kumtegemea rafiki wa kweli na kupata msaada, lakini asitazamie msaada huo upite kiasi kwamba rafiki huyo afilisike (17-18). Mtu ambaye kwa njia ya matendo ya kinyume hujiendeleza ili aweze kujivunia hali ya daraja la juu anachokoza uangamizi (19-20). Upumbavu huleta huzuni, na huzuni ya daima huharibu afya ya mtu. Kinyume chake, uchangamfu humsaidia mtu kuwa na afya njema (21-22). Watu wasio na hatia huteswa na   maafisa   wanaodai   rushwa,   na   wazazi   wa mpumbavu hupata huzuni kwa sababu ya upumbavu wa mwana wao. Mpumbavu hutanga tanga bila makusudi, lakini mwenye bidii hufikiri matendo yake yote kwa akili (23-26). Alama ya hekima ni kufikiri kabla ya kusema (27-28).

Kutajwa kwa rushwa na ushuhuda wa uongo mara nyingi kunadokeza jinsi mahakama yalivyochafuka kwa mambo hayo wakati wa kuandikwa mithali hizo; taz.l4:5,25; 17:8,15,23,26; 18:5; 19:5,9,28).

Nguvu ya kweli (18:1-24)
Inawezekana kwamba mtu anaamini sana mashauri yake mwenyewe hata akawaacha marafiki zake wa zamani, akishindwa kujadiliana na watu, naye huwa kipofu kwa mawazo ya watu wengine. Watu wanaodharau wengine, wenyewe wataaibishwa (18:1-3). Maneno ya mwenye hekima huburudisha, lakini maneno ya mpumbavu au ya mpiga domo huharibu (4-8). Mtu aachaye kazi bila ya kuimaliza hufanana na mtu anayeharibu kilichotengenezwa (9). Mtu anayemtegemea Mungu anajua kwamba yu salama; ila mtu ategemeaye mali yake anafikiri kwamba yu salama, lakini siku moja atatambua kwamba kiburi huleta uharibifu (10-12).

Nguvu ya akili na uthabiti wa roho ni bora katika vita vya maisha kuliko nguvu za kimwili. Mwenye hekima husikiliza ushauri kutoka kila upande uwezekanao kabla ya kutoa uamuzi wake. Lakini mara nyingine watu wanaweza kujaribu kupata kibali kwa njia ya kutoa zawadi, na mara nyingine labda wanapaswa kupiga kura ili kuamua jambo gumu (13-18). Mtu anaweza kuwa rafiki sana au adui mkali wa mtu kutokana na jinsi anavyotendewa. Matunda ya maneno ya mtu humrudia mwenyewe kwa wema au kwa ubaya (19-21). Urafiki wa kweli hauvunjiki upesi wala hautofautishi baina ya tajiri na maskini. Lakini mke mwema ni rafiki bora kuliko wote (22-24).

Mafundisho yanayokubaliwa na yanayodharauliwa (19:1-29)
Ni muhimu zaidi kuwa mnyofu katika maadili kuliko kuwa tajiri, kutimiza mambo kwa uangalifu kuliko kuyamaliza kwa haraka ya kuhangaika. Watu wasimlaumu Mungu kwa shida waliyojipatia wenyewe kwa njia ya makosa yao (19:1-3).

Mara nyingi sababu ya tajiri kuwa na marafiki wengi ni kwamba, 'marafiki' hao hutegemea kupata faida yao binafsi kutokana na mali au uwezo wa tajiri huyo (4-6). Upande mwingine, maskini hupoteza marafiki zake, ingawa kwa namna fulani ni tajiri akiendelea kuwa na hekima yake (7-8). Afadhali kila mtu aishi kadiri ya hali na uwezo wake katika jumuia, ingawa kutojali ukweli siku zote ni vibaya (9-10). Akiwa na busara ya mtu aliyekomaa, hatakubali kuchukuliwa na hasira upesi, naye atajua jinsi ya kujitawala (11-12).

Upumbavu, ugomvi, uvivu na ukosefu wa nidhamu ya wazazi huharibu furaha ya familia. Matendo yenye hekima, huruma na uthabiti wa wazazi hujenga nyumba hiyo (13-18). Mtu mwenye tabia ya harara anaonekana kama hawezi kujifunza kamwe, na matokeo yake, daima hujiletea taabu (19-20).

Mungu huongoza mambo ya maisha ya watu, naye anatazamia kwao uaminifu na utii. Anawabariki wale wanaomtii, lakini si wale walio wavivu (21-24). Mapigo ya fimbo mara nyingine ni njia ya pekee ya kumrekebisha mpumbavu, lakini mtu mwenye busara husikiliza akionywa na kujifunza kutokana na makosa yake (25-29).

Uaminifu (20:1-30)
Mtu mwenye hekima hatakuwa mlevi, hatawachokoza wenye mamlaka bila sababu maalumu, atakwepa ugomvi, naye atafanya kazi ili ajipatie riziki yake (20:1-4). Pia atakuwa na uwezo wa kutambua mawazo na makusudi ya ndani ya mtu anayeshughulika naye (5). Watu wengi hujisifu kuhusu uaminifu wao, lakini wachache tu ni waaminifu kweli. Kuishi katika uaminifu ni njia bora kwa mtu kuwahakikishia watoto wake maisha bora kwa wakati wa usoni (6-7). Mfalme hujifunza kutokana na uzoefu wake kuamua kati ya wema na ubaya katika mambo yanayoletwa mbele yake ili atoe uamuzi, lakini pia anajua kwamba moyo wake, sawasawa na mioyo ya wanadamu wote, hauwezi kuwa bila dhambi (8-9).

Mungu huchukia udanganyifu. Iwapo hata mwanadamu kwa njia fulani anaweza kutambua hali ya moyo wa mtu mwingine kutokana na matendo yake, sembuse Mungu aliyewaumba wanadamu (10-12). Mfanyakazi mwaminifu huridhika akijua kwamba riziki yake anapata kwa njia ya haki; lakini mnunuzi mwenye hila apataye kitu bora kwa bei rahisi (kwa sababu alikilaumu mbele ya mwenye mali), kujisifu kwake hakuna muda mrefu. Watu wengine hawaaminiki, kwa hiyo mtu aangalie sana wakati wa kukopesha pesa, naye ahakikishe kufanya usalama fulani wa dhamana au rehani ili arudishiwe mali yake (13-17). Mtu mwenye hekima husikiliza ushauri, hukwepa porojo na kuwaheshimu wazazi wake jinsi inavyompasa (18-20).

Kutotulia humsababisha mtu kukosa, ikiwa ni katika kungojea urithi wa agano fulani, au katika kutaka kumwona mkosaji aadhibiwe, au katika kuahidi nadhiri kubwa kwa haraka. Utulivu humwezesha mtu kumngojea Mungu naye ataongoza mambo yote (21-25). Adhabu za mfalme zinaweza kuwa kali, lakini lazima ziwe na haki (26). Inafaa dhamiri ya mtu imwonyeshe makosa yake ili aweze kujirekebisha, lakini mara nyingine dhamiri yake haifanyi kazi vizuri, na hapo adhabu ya kuumiza zaidi inatakiwa ili kusawazisha makosa yake (26-30).

Mungu hushughulika na wanadamu (21:1-31)
Kama vile Mungu anavyoongoza mkondo wa mito, ndivyo anavyoongoza uamuzi wa watawala wa mataifa kadiri ya makusudi yake (21:1). Mungu anajua makusudi ya wanadamu naye hatakubali sadaka zao, iwapo mawazo na matendo yao ni kinyume (2-4). Mafanikio yanayotokana na bidii ni thawabu njema; mafanikio yanayotokana na ubahili, uongo na ujeuri ni mtego uletao mauti (5-8). Watu wengine hufanya maisha kuwa magumu sana kwa wale waishio pamoja nao katika nyumba moja, na wengine wanatazamia kufanya uovu kwa makusudi po pote wanapoweza. Watajiharibu wenyewe, lakini wenye haki watafurahia baraka (9-12).

Mtu anaweza kuishi kwa ajili ya faida yake binafsi tu, akiwadharau wenye dhiki na kuwapa rushwa wenye uwezo ili apate kitu cho chote anachokitaka ili aishi katika starehe. Ni haki kama siku moja atapata shida kutokana na ubinafsi wake na kutokuwa mwaminifu (13-17). Hivyo akiteswakwa ajili ya uovu aliomkusudia mtu asiye na hatia, mtu mwovu huwa fidia au badala ya mwenye haki (18). Mwenye hekima huweka akiba kwa ajili ya siku zijazo, wakati huo huo akitambua kwamba, njia ya pekee ya kupata mali idumuyo ni kutenda haki na fadhili (19-21).

Hekima ina faida zaidi kuliko nguvu ya kijeshi, na kutawala ulimi ni silaha bora dhidi ya matatizo (22-23). Matendo ya kidini yakitimizwa kwa makusudi ya kinyume ni chukizo kwa Mungu, pamoja na kiburi, uvivu na tamaa ya ubinafsi (24-27). Mtu anapaswa kutoa ushuhuda maalumu kuhusu mambo anayoyajua, wala si kuonyesha sura yenye ujasiri tu ili atafute heshima ya watu (28-29). Ni bure kabisa kushindana na Mungu, pia ni bure kushindana au kupiga vita bila Yeye (30-31).

Watoto na watu wazima (22:1-16)
Watu wanatofautiana katika hali na sifa zao, lakini wanapaswa kuheshimiana wakijua kwamba wote ni viumbe vya Mungu bila tofauti ya thamani yao (22:1-2). Mwenye hekima hutimiza matendo yake kwa uangalifu na unyenyekevu. Hulea watoto wake ili awaandae kwa maisha yanayowakabili (3-6). Mtu akopaye atakuwa chini ya mamlaka ya mkopeshaji, na hali hiyo inaweza kusababisha kuonewa kwa maskini na matajiri. Lakini dhuluma ya namna hiyo itaadhibiwa, ambapo fadhili italeta thawabu (7-9).

Watu wanapojaribu kufanya kazi pamoja kama kikundi, lazima waelewane na kupatana. Ni afadhali kuondokana na mtu aletaye ugomvi daima kuliko kuendelea naye. Upande mwingine, mtu asemaye kweli huleta faida (10-11). Mungu anataka watu wafanyao mambo kadiri ya ujuzi na ukweli. Hapendezwi na mtu mvivu ambaye siku zote hujitetea tu, au mwanamke asiye na heshima ambaye hukosesha watu wengine kwa umalaya wake (12-14). Ujinga wa kitoto unaweza kurekebishwa na nidhamu ya wazazi. Ubahili wa watu wazima unaowaonea maskini na kuwapa rushwa matajiri kutaadhibiwa (15-16).

</

0 comments: